Mohammad Javad Zarif Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameyasema hayo leo asubuhi katika kikao cha Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, Bunge la Iran. Zarif amesema pamoja na kuwa Wizara ya Mambo ya Nje haina jukumu la moja kwa moja la kiuchumi lakini inatekeleza mkakati wa kuondoa matatizo ya kiuchumi yaliyosababishwa Marekani nchini.
Zarif amesema hatua ambazo Marekani inazichukua dhidi ya Tehran ni za mabavu na ni ugaidi wa kiuchumi. Ameongeza kuwa, msingi wa sera hizo za Marekani ni mashinikizo ya juu zaidi dhidi ya Iran.
Katika kikao hicho, Zarif ametoa maelezo zaidi kuhusu matukio ya kimataifa na sera za kigeni za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ambapo amebaini kuwa Marekani hivi sasa iko katika vita vya pande zote dhidi ya Iran. Ameongeza kuwa, Marekani inaiarifisha Jamhuri ya Kiislamu kama tishio dhidi ya usalama na inajaribu kuibua muungano dhidi ya Iran kwa kutoa taarifa bandia na kuwashinikiza marafiki wa Iran. Zarif amesema, kwa muqawama na mapambano ya wananchi na viongozi wa Iran, njama hizo za Marekani zitagonga mwamba.
Amesema kuwa, kwa utumiaji mabavu wa Marekani, tokea Januari 2018 hadi wiki iliyopita, kumefanyika vikao vinne maalumu vya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa lengo la kuishinikiza Iran. Ameongeza kuwa Marekani imetengwa baada ya wanachama wa baraza hilo kukataa kuunga mkono sera zake hasimu.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema Marekani haitafikia malengo yake dhidi ya Iran na kuongeza kuwa, moja ya hatua ambazo zinaweza kupunguza mashinikizo ya vikwazo ni kuondolewa sarafu ya dola katika mabadilishano ya kibiashara na hivyo Iran inafutilia kadhia hii.